hk CONTACTS

hk CONTACTS

Friday, May 17, 2013

MCHEZA FILAMU ZA NGONO SEHEMU YA 7.








Miaka saba ilikuwa imekwenda sana tangu kipindi kile ambacho mvulana Daniel alipokuwa ameangukia katika mapenzi ya msichana Katie katika kipindi kile ambacho walikuwa wakiishi mitaani. Katika kipindi hiki hakuwa nchini Marekani tena, alikuwa akitembea katika nchi mbalimbali kama baharia ambaye alikuwa akifanya kazi katika meli kubwa ya Metropoza iliyokuwa ikizunguka sehemu mbalimbali duniani.
Picha za Katie alikuwa akiziangalia mara kwa mara, alimkumbuka sana msichana huyo kutokana na uzuri mkubwa ambao alikuwa nao, alimkumbuka kwa kila kitu japokuwa alijua fika kwamba msichana huyo kwa sasa alikuwa akiigiza filamu za ngono ambazo zilikuwa zikimuingizia fedha za kutosha.
Alikuwa amefanya kazi ya ubaharia kwa miaka zaidi ya saba, uzoefu wake mkubwa ambao alikuwa nao Daniel ndio ambao uliwafanya hawa nahodha wa meli hiyo kumpa uongozi huku akimlipa kiasi kikubwa cha fedha. 
Daniel alikuwa akiyakumbuka vizuri maisha yake ya nyuma ambayo alikuwa ameishi zamani, yalikuwa maisha ya shida ambazo kila siku zilikuwa zikimpelekea kutafuta fedha maishani mwake pasipo kujali ni aina gani ya shida ambazo angeweza kukutana nazo.
Maishani mwake alipenda sana maendeleo, alitamani pia kuwa na msichana Katie ambaye alikuwa akimfahamu toka walipokuwa wadogo, wakicheza wote na kufanya mambo mengi pamoja. Katika kipindi kile, japokuwa Katie alikuwa akijitahidi kutokumuonyeshea mapenzi ya wazi lakini Daniel alikuwa na uhakika wa asilimia mia moja kwamba msichana yule alikuwa akimpenda sana.
Kwake, kitendo cha Katie kujiunga na uigizaji wa filamu za ngono ukaonekana kumuumiza sana lakini hakujua ni kitu gani ambacho alikuwa akitakiwa kukifanya zaidi. Kama kumshauri, alikuwa amemshauri sana lakini Katie hakuonekana kubadilika.
Daniel alikuwa na uhakika kwamba katika kipindi hicho Katie hakuwa akikumbuka kitu chochote kile ambacho kilikuwa kimepita katika maisha yao. Ingawa alikuwa akiendelea kufanya kazi ya ubaharia lakini akili yake wala haikuacha kumfikiria Katie ambaye kadri siku zilivyozidi kwenda mbele ndivyo alikuwa akiendelea kunawili.
Kwa kipindi hiki, Daniel alikuwa mnyonge sana japokuwa alikuwa na kiasi kikubwa cha fedha, maisha yake katika kipindi hiki hayakuwa nchini Marekani tena, alikuwa akiishi nchini Uingereza katika jiji la Newcastle ambako huko alikuwa amenunua nyumba kubwa na ya kifahari.
Fedha ambazo alikuwa amezipata katika ubaharia wake ndizo ambazo akaamua kufungulia mghahawa ambao ulikuwa ukitumiwa sana na wachezaji wa mpira wa klabu ya Sunderland ambao walikuwa wakifika sana mahali hapo kwa ajili ya kupata kifungua kinywa na hata chakula cha jioni hasa mara baada ya kutoka mazoezini.
Ingawa maisha ya Uingereza hakuyapenda sana kutokana na baridi lakini akaamua kuvumilia tu. Kwake alijiona kuwa mtafutaji ambaye alitakiwa kukaa sehemu yoyote ile katika dunia hii mpaka pale ambapo angebadilisha maisha yake na kuishi kama tajiri mmoja mkubwa nchini hapo na kurudi nchini Marekani na kununua nyumba na maisha ya kifahari kuanza rasmi.
Maisha ya Daniel yalikuwa yamelenga mambo mengi sana, hakutaka kutumia fedha zake vibaya, alikuwa akiishi nchini Uingereza kama mgeni tu na hivyo kuna siku angehitaji kurudi nchini kwake. Kutokana na kuanza kuingiza fedha nyingi, wasichana mbalimbali wa hapo Newcastle walikuwa wakipenda kumfuatilia kwa lengo la kuwa nao lakini Daniel hakukubaliana nao, kazi yake ilikuwa ni kutembea nao kwa zamu na kuwaacha tu.
Maishani mwake hakutaka kuwa na msichana yeyote yule zaidi ya Katie ambaye bado alikuwa akiigiza filamu za ngono kama kawaida yake. Miezi ikakatika na ndipo hapo Daniel aipojiona kuwa na utayari wa kurudi nchini Marekani kwa ajili ya kuendelea na maisha katika nchi hiyo huku tayari akiwa ameingiza zaidi ya kiasi cha paundi milioni tano.
Kitu cha kwanza mara baada ya kufika nchini Marekani ni kuanza kufungua biashara nyingi ambazo zilionekana kumuingizia fedha na kisha kuanza kumtafuta Katie simuni. Msichana huyo hakuwa akipatikana kabisa jambo ambalo lilimfanya kuendelea kumtafuta zaidi na zaidi. Ingawa alikuwa akiiangalia mikanda ya filamu ya Katie ambayo alikuwa akiigiza akifanya mapenzi na wanaume mbalimbali lakini bado alikuwa akihitaji kuwa nae katika maisha yake.
Baada ya kipindi kirefu kupita, Daniel akaja kupata taarifa ambayo ilionekana kumshtua sana, taarifa ambayo ilimfanya kuchanganyikiwa kupita kawaida. Katie alikuwa akitarajia kufunga ndoa, aliuhisi moyo wake ukichomwa na msumali wa moto na kisha tundu hilo kumwagiwa tindikali.
Hakuziamini taarifa zile jambo ambalo likamfanya kutembelea katika website ya Katie na kuangalia. Kile ambacho alikuwa amekioa katika magazeti mbalimbali nchini Marekani kilikuwa sawa sawa na kile ambacho alikuwa amekikuta katika website ile.
Daniel akajiona akikosa nguvu kabisa, akaanza kupiga hatua kuelekea katika kochi na kisha kutulia. Mawazo yakaanza kumuandama kichwani mwake. Katika maisha yake, hakuona kama kulikuwa na mtu ambaye alitakiwa kumuoa Katie na kuishi nae tofauti na yeye, jambo lile likaonekana kumtia hasira sana.
Alichokifanya ni kuanza kupeleleza juu ya mwanaume ambaye alikuwa akitarajiwa kufunga ndoa na Katie. Alijitahidi kumtafuta zaidi na zaidi lakini hata picha yake akashindwa kuipata mpaka siku ya harusi ilipofika na watu hao kufunga ndoa.
Daniel akaonekana kuchanganyikiwa zaidi, alijua fika kwamba ndoto zake za kutaka kuishi na Katie hapo baadae zilitakiwa kufutika kunzia muda huo. Kila siku alikuwa akishinda chumbani akilia huku picha za Katie ambazo alipiga nae kipindi cha nyuma walipokuwa mitaani utotoni zikiwa mikononi mwake.
Mapenzi yake yalikuwa makubwa kwa Katie, alimpenda sana kuliko msichana yeyote katika dunia hii. Alimuona kuwa msichana ambaye alihitaji thamani kubwa sana katika maisha yake. Hakuwa radhi kuwa na msichana mwingi, msichana ambaye alikuwa akimpenda na kumhitaji alikuwa Katie tu.
Alipokuja kuiona picha ya Gibson kwamba ndiye alikuwa mume halali wa Katie, Daniel akapigwa na mshangao. Kwanza akaanza kumwangalia vizuri Gibson huku akijaribu kujilinganisha nae, hakuwa akifanana na Gibson hata kidogo.
Hapo hapo akaanza kumchukia Gibson, hakujali kama Katie ndiye ambaye alikuwa amemtongoza Gibson na hatimae kuoana, yeye alichokuwa akikijali kwa wakati huo ni kuendelea chuki kwa Gibson tu huku ngozi ya Gibson kuwa nyeusi ndicho kilikuwa kitu ambacho kilimkasirisha zaidi na zaidi.
Daniel hakuwa radhi kumuona Gibson akila raha pamoja na mwanamke ambaye alikuwa akimpenda tangu utotoni, hakuwa radhi kuona Gibson akila raha na msichana ambaye alikuwa amefanya nae mapenzi sana mitaani, hakuwa radhi kuona Gibson akila raha na msichana ambaye alikuwa akiishi nae kwa karibu zaidi ya mtu yeyote, kitu alichokuwa akikitaka kwa wakati huo ni kuyarudisha mapenzi ambayo yalikuwa yamepotea na kusahaulika tu.
Hakukuwa na njia nyingine zaidi ya kuyarudisha mapenzi ya Katie kwake zaidi ya kufanya kitu kimoja tu, cha kumuua Gibson. Aliamini kwamba kama asingefanya hivyo, basi kwake lingekuwa jambo gumu sana kuweza kumpata Katie ambaye alionekana kuwa kwenye mapenzi mazito na mwanaume huyo.
Alichokifanya ni kuanza kuandaa mipango kabambe, mipango ambayo ingemmaliza Gibson na kisha kumsahaulisha katika kichwa cha Katie na baada ya hapo angeweza kumfuata Katie na kumwambia juu ya jinsi alivyokuwa akiendelea kujisikia ndani ya moyo wake, amkubalie, amuoe na hatimae kutimiza ndoto yake ambayo alikuwa akiiota kila siku.
Alichokifanya ni kuwakodisha vijana ambao walitakiwa kuucheza mchezo ule kwa makini sana bila kukosea sehemu yoyote ile. Vijana wakakubaliana nae kwa malipo makubwa ambayo wala hayakuonekana kuwa tatizo kwa Daniel ambaye kwa kipindi hicho alikuwa na fedha za kutosha.
Sehemu ambayo ilitakiwa Gibson auawe ilikuwa ni Texas, jiji ambalo kwa kiasi fulani lilionekana kuwa kama jangwa. Kila kitu kikapangwa, vijana wakaomba siku mbili za kujiandaa na hatimae baada ya hapo kukamilisha kila kitu.
“Kwa hiyo baada ya kumteka tumuue au tukusubirie wewe umuue?” Kijana mmoja alimuuliza Daniel.
“Nataka kumuua mimi mwenyewe. Tena kwa mkono wangu” Daniel aliwaambia.
“Sawa sawa. Usijali. Tutakamilisha kila kitu” Kijana yule alimwambia Daniel na kisha kuondoka.
*****
Maisha ya mapenzi bado yalikuwa yakiendelea kama kawaida kwa wapendanao, Gibson na Katie. Walikuwa na ukaribu mkubwa sana huku kila siku wakiwa wanatawala vyombo vya habari nchini Marekani. Bila kupenda, Gibson akaanza kuwa maarufu nchini Marekani jambo ambalo lilimpelekea kuanza kujulikana kila sehemu hasa katika nchi nyingine.
Bado malengo yake yalikuwa ni yale yale, kwa msichana Katie, kitu ambacho alikuwa akikihitaji ni kupata fedha tu. Alikuwa amekwishagundua kwamba Katie alikuwa na fedha nyingi, hivyo alijitahidi kuonyesha kila kitu hasa mapenzi ya dhati ili mwisho wa siku apate kile ambacho alikuwa amekipanga kukipata.
Katie akaonekana kuanza kubadilika, akajifanya kuacha kuigiza filamu za ngono jambo ambalo likaonekana kuwakasirisha watu wengi nchini Marekani ambao walikuwa na kiu ya kutaka kumuona akiigiza filamu zile.
“Sasa tufanye nini?” Bwana Donald, mkurugenzi wake alimuuliza.
“Nitakuwa nikiigiza kama kawaida” Katie alijibu.
“Sasa akiziona itakuwaje?”
“Usihofu. Nitakuwa namwambia kwamba hizo zilikuwa filamu za zamani ambazo zilikuwa zimekwishatengenezwa hata kabla ya kukutana nae” Katie alijibu huku akitabasamu.
“Utaweza kweli kumshawishi hadi akubaliane nawe?”
“Ndio. Mwanamke atabakia kuwa mwanamke, hatosema kitu chochote kwa mwanamke, atakubaliana nami tu” Katie alijibu.
Alichokifanya baada yakufika nyumbani ni kumsubiri Gibson atoke kazini na ndipo hapo alipomwambia kila kitu kilichokuwa kinaendelea. Japokuwa Gibson alijifanya kuumia lakini akakubaliana nae jambo ambalo lilimfanya Katie kumpa mapenzi moto moto.
“Au tufanye kitu kimoja ili kukupa uhuru” Gibson alimwambia Katie.
“Kitu gani?”
“Wewe igiza tu filamu zako. Ila nataka kukuwekea sharti moja tu” Gibson alimwambia Katie.
“Sharti gani?”
“Hakikisha cd hizo hazionekani machoni mwangu. Yaani kama ukitaka kuziangalia ziangalie kwa siri. Umenielewa mke wangu?” Gibson alimuuliza Katie.
“Nimekuelewa mpenzi na ninashukuru kwa ruhusa yako. Nakuhakikishaia kila kitu kitakuwa kama ulivyoniambia” Katie alimwambia Gibson ambaye akili yake ilikuwa ikifikiria fedha tu na huku akiwa ameshaanza kutuma fedha kisiri katika akaunti yake iliyokuwa nchini Tanzania.
******
Vijana watatu wakajipanga vilivyo huku lengo lao katika kipindi hicho likiwa ni kukamilisha kazi ambayo walikuwa wamepewa na Daniel ya kumteka Gibson na kisha kumpeleka sehemu ya siri ambako huko wangempigia simu bosi wao na kisha kumueleza kila kilichoendelea.
Wakaandaa bunduki zao, walikuwa wamejiandaa na utekaji nyara ambao mara kwa mara ulikuwa ukifanyika sana nchini Marekani hasa kwa watoto wa watu wenye fedha na watekaji hao kudai kiasi kikubwa cha fedha.
Walichokuwa wameelekezwa ni mahali ambapo kulikuwa na uwezekano wa Gibson kupatikana na kisha kumpeleka sehemu yoyote ile ambayo kusingekuwa rahisi kwa Katie kuweza kuwasiliana nae mpaka pale atakapouawa na mkono wa Daniel.
Mipango ilikuwa imekamilika kabisa, saa 4:18 asubuhi, gari aina ya Mc Lloyd lilikuwa limesimama mbali kidogo na nyumba kubwa aliyokuwa akiishi Katie na Gibson katika mghahawa mmojawapo wa Mc Donald. Vijana wale waliendelea kusubiri zaidi na zaidi huku kengo lao likiwa ni kutaka kumuona Gibson akitoka ndani ya nyumba ile kwa ajili ya kufanya kile ambacho walikuwa wametumwa.
Saa 6:24, gari ndogo aina ya Ferrari yenye viti viwili ikaanza kutoka ndani ya nyumba ile. Vijana wale wakatoka katika mghahwa ule na moja kwa moja kulifuata gari lao na kuingia ndani. Wakaanza kulifuatilia gari lile kwa mwendo wa taratibu uliojaa angalizo kubwa.
Bunduki zao zilikuwa tayari, walikuwa wamejiandaa kwa kitu chochote kile ambacho kingetokea mahali hapo, kitu ambacho kingewafanya kutofanikisha mpango ambao walikuwa wameupanga kuufanya kwa wakati huo.
Waliendelea kulifuata gari lile la kifahari mpaka lilipoingia katika duka moja kubwa la nguo ambalo lilikuwa likitumika sana na masupastaa au na watu ambao walikuwa na fedha nyingi na za kutosha. Vijana wale hawakutaka kuingia, wakasubiri nje huku wakiwa garini mwao.
Muda ulikuwa ukizidi kwenda zaidi na zaidi lakini hakukuwa Gibson na Katie hawakuweza kutoka ndani ya duka lile, waliendelea kusubiri zaidi na zaidi na baada ya dakika arobaini na tano, wakawa wanatoka huku mikononi mwao wakiwa na mifuko miwili mikubwa ambayo waliipeleka ndani ya gari lao na kisha kuingia na kuanza kuondoka mahali hapo.
Vijana wale hawakutaka kusubiri mahali hapo, walichokifanya ni kuanza kuwafuatilia kwa mara nyingine tena. Waliendelea kuwafuatilia zaidi na zaidi mpaka kufika katika barabara ya mtaa wa Vikingstone ambako hakukuwa na magari mengi kabisa na kisha kulipita gari lile na kulisimamisha gari lao mbele na kuteremka kwa kasi ya kikomandoo.
Katie ambaye alikuwa katika usukani alibaki akiwa amepigwa na mshangao mkubwa ulioambatana na mshtuko, hakuonekana kufahamu ni kitu gani ambacho kilikuwa kinaendelea mahali hapo, hata kabla hajajua afanye kitu gani, vijana wale wakawa wamekwishalifikia gari lile na kuvivunja vioo vya dirishani kwa kutumia vitako vya bunduki zao.
Hawakutaka kuuliza kitu chochote kile, kutokana na kutokuwa na uwepo wa watu katika barabara ya mtaa ule wa kifahari iliwafanya kuwa na uhuru mkubwa wa kuwafanya chochote walichotaka kufanya. Mara ya kwanza Gibson alitaka kuonyesha ubabe lakini alipoziona bunduki mbele ya macho yake, akatulia.
Wakateremshwa garini mule na kisha kupelekwa katika gari lile walilokuja nao vijana wale na kisha safari ya kuelekea katika sehemu ambayo walitakiwa kuwapeleka kuanza kwa wakati huo. Muda wote Gibson na Katie walikuwa wakitetemeka kwa hofu, watu ambao walikuwa nao ndani ya gari lile walionekana kuwa watu wenye roho mbaya ambao muda wote walikuwa wakinuka damu.
Gari likachukua barabara ya Melville 46 na kisha kuanza kuelekea katika mji wa Baldwin huku lengo lao kubwa katika kipindi hicho ni kwenda kwenye jiji la Texas ambalo lilikuwa katika upande wa mashariki wa jiji hilo la New York karibu kabisa na mji wa Greenvale.
Mwendo wa gari lao haukuwa wa kasi sana, walikuwa wakizihofia kamera za barabarani ambazo zingewafanya kuwafuatilia zaidi endapo mwendo wao ungeonekana kuwa wa kasi zaidi tofauti na magari mengine. Waliendelea na safari ile kwa muda wa dakika kumi na ndipo hapo walipochukua barabara ya magari yaendayo kasi ya Hoy Hills huku wakiwa na dakika thelathini kabla ya kufika katika jiji la Texas.
Muda wote huo, hakukuwa na mtu ambaye aliufungua mdomo wake, wote walikuwa kimya kabisa ndani ya gari lile. Katie alitamani kuuliza juu ya kitu ambacho kilikuwa kinaendelea mahali hapo lakini hakupewa jibu lolote lile zaidi ya wote kupewa onyo la kutokuongea kitu chochote kile.
Huku gari likiendelea kwa mwendo wa kasi ya zaidi ya kilometa themanini kwa saa, simu ya kijana mmoja katika ya vijana wale watatu ikaanza kuita
“Mko wapi?” Sauti ya Daniel iliskika.
“Tupo katika barabara ya Hoy Hills” Kijana yule alijibu.
“Mko nae hapo?”
“Ndio. Tupo nao wote” 
“Ina maana hadi Katie?” Dany aliuliza huku sauti yake ikisikika kujaa mshangao.
“Ndio bosi’
“Hapana. Huyo msichana simuhitaji kabisa. Mshusheni arudi zake. Ila mshusheni katika sehemu ambayo hamtoonekana kirahisi” Daniel alisema.
Kila kitu ambacho Daniel alikuwa ameamuru kwa wakati huo ndicho ambacho kilitakiwa kufanyika kwa haraka sana, tena bila ya kuulizwa swali lolote lile. Gari lilipofika katika kituo cha mafuta, Katie akateremshwa na kisha kuanza kupelekwa bafuni ambako kijana mmoja alikuwa pembeni yake akiigiza kuwa kama mpenzi wake ili kuwaondoa wasiwasi watu wachache ambao walikuwa wakipishana nao.
Walipofika chooni, Katie akafungwa kamba katika bomba la maji na kisha kijana yule kurudi garini na kuendelea na safari yao huku Gibson akizidi kutetemeka kadri muda ulivyokuwa unazidi kwenda mbele.
Baada ya dakika zaidi ya arobaini wakaingia katika jiji la Texas ambalo lilikuwa likionekana kuwa kama jangwa. Jiji hili ndilo ambalo lilikuwa limepakana kwa ukaribu sana na nchi ya Mexico na watu wengi ambao walikuwa wakiishi katika jiji hilo walikuwa wakitoka katika nchi hiyo huku muda mwingi wakiwa wanavaa makofia makubwa ya Malboro huku wakijulikana sana kwa jina la Cow Boys.
Hali ya hewa haikuwa ya baridi sana kama ilivyokuwa jijini New York, kutokana na sehemu kubwa kuwa jangwa, hali ya joto ndio ambao ilikuwa ikitawala sana hasa katika nyakati hizo za mchana. Moja kwa moja wakaanza kuelekea katika sehemu ambayo ilikuwa na jumba kubwa bovu bovu na kisha kumuingiza humo.
Gibson akatulia ndani ya jumba lile ambalo lilionekana kuwa na hadhi ya kujengwa katika sehemu kama ile ya jangwa huku vijana wale wakiwa nje wakimsubiria Daniel ambaye alikuwa amewataarifu kwamba ni lazima angefika mahali hapo haraka iwezekanavyo.
Ndani ya dakika hamsini, gari la kifahari aina ya Penina 11 likaanza kuingia ndani ya eneo hilo na kisha Daniel kuteremka huku akiwa amevalia suti nyeupe na macho yake yakiwa yamefunikwa na miwani ya mwanga. Akawasalimia vijana wale huku uso wake ukionyesha kuwa na furaha na kisha kukabidhiwa bunduki na kuanza kupiga hatua kuingia ndani ya jumba lile.
Uamuzi ambao alikuwa ameuweka Daniel kwa kipindi hicho ulikuwa ni uamuzi mmoja tu ambao wala haukuhitaji hata ushauri kutoka kwa mtu yeyote yule, hakutaka maelezo yoyote yale, kadri alivyokuwa akipiga hatua kuufuata mlango wa jumba lile na ndivyo ambavyo hasira zake zilivyokuwa zikizidi kumpanda. Kichwa chake kilikuwa kikimfikiria Katie, alimuona Gibson kuwa kiziuzi kikubwa kwa yeye kuwa na msichana yule ambaye alikuwa akimpenda kuliko mwanamke yeyote yule.
“Hakuna maelezo, hakuna maswali na wala hakuna mahojiano, hapa ni kuua tu” Daniel alisema huku akiwa amekwishaingia ndani ya jumba lile huku mkono ulioshika bunduki ile ukimtetemeka kwa hasira kali. Mtu ambaye alikuwa akimwangalia katika kipindi hicho, alikuwa Gibson ambaye alikuwa akitetemeka kupita kawaida.
“Ninakuua” Daniel alijisemea huku akimnyooshea Gibson bunduki ile.
“Paaaaa...paaaaaa...paaaaa...” Risasi zilisikika zikitoka katika bunduki aliyoishika Daniel huku uso wake ukionyesha tabasamu pana.

Je nini kitaendelea?
Je Gibson ameuawa?
Je Daniel atafanikiwa kumpata Katie kama anavyotaka?
Je ni nini kitaendelea katika maisha yao hawa?
Itaendelea jumatatu wikiend tamthilia inapumzika.
story hii kali imedhaminiwa na DICK SOUND,ZANNEL BONGO LADIES WEAR,MAC AUTO ACCESSORIES na FACEBOOK TAKE AWAYwauzaji wa chips tamu kinondoni.
Maoni 0786435543.

No comments:

Post a Comment