hk CONTACTS

hk CONTACTS

Thursday, May 30, 2013

MCHEZA FILAMU ZA NGONO SEHEMU YA 14



 Msichana Katie alikuwa akiendelea kufanyakazi zake kama kawaida huku akionekana kutokuwa na wasiwasi hata kidogo. Muda wote alikuwa bize akifanya kazi zake lakini huku mawazo yake yakiwa yanamfikiria Gibson. Mapenzi ambayo alikuwa nayo kwa Gibson yalikuwa makubwa, pengo kubwa ambalo alikuwa nalo moyoni mwake wala halikuweza kuzibika hata mara moja.
Gibson alikuwa ameuumiza moyo wake kupita kawaida, muda mwingi alikuwa akionekana mpweke, muda wote alikuwa akiomba Mungu vijana ambao alikuwa amewatuma nchini Tanzania wafanye kazi kama ambavyo aliitaka ifanyike. Muda mwingi alikuwa akiwasiliana nao kwa kutumia mtandao wa simu wa Kimataifa wa Tricom ambao ulikuwa ukitumiwa sana na wazungu kutoka Marekani na barani Ulaya.
Kila alipokuwa akiwasiliana nao, aliambiwa kuwa mvumilivu kwa sababu kila kitu kilikuwa kikiendelea kama kilivyotakiwa kiwe. Katie hakuwa na jinsi, kitu ambacho alikuwa akikifanya kwa wakati huo ni kuendelea kuwa mvumilivu kama kawaida. 
Katie aliendelea kuwa kwenye lindi la mawazo mpaka kipindi kile ambacho akaanza kupokea maua mbalimbali ya kimapenzi pamoja na zawadi nyingi zilizokuwa zikihusu mapenzi. Katie alionekana kushangaa, hakujua ni mtu gani ambaye alikuwa akimtumia zawadi hizo ambazo zilikuwa zikija mfululizo, yaani asubuhi, mchana na jioni.
Kutokana na hali ambayo alikuwa nayo katika kipindi hicho wala hakutaka kujali sana kuhusiana na maua hayo na wala hakutaka kumjua mtu ambaye alikuwa akimtumia vitu hivyo vyote. Mawazo yake kwa wakati huo yalikuwa yametulia kwa mtu mmoja tu, mtu ambaye alikuwa amemuachia tundu kubwa moyoni mwake, tundu ambalo lilikuwa likiendelea kuuma kadri siku zilivyozidi kwenda mbele.
Zawadi ziliendelea kumiminika nyumbani kwake zaidi na zaidi mpaka kufikia kipindi ambacho akatamani kumuona mtu huyo ambaye alikuwa akitumia muda mwingi kumtumia zawadi mbalimbali. Alichokifanya ni kumpigia simu kupitia namba zake ambazo alikuwa akiziambatisha katika zawadi mbalimbali alizokuwa akimletea.
Siku iliyofuata, mwanaume huyo, Daniel akafika nyumbani kwa Katie na moja kwa moja kukaribishwa ndani. Katie hakuonekana kuamini, mwanaume ambaye alikuwa ameingia ndani ya nyumba yake alikuwa akimfahamu vilivyo, alikuwa Daniel, mtu ambaye alikuwa mpenzi wake na ndiye alikuwa mtu ambaye aliutoa usichana wake katika miaka ya nyuma, kipindi ambacho walikuwa wakiishi mitaani.
Kwa mbali, uso wake ukaanza kuonyesha tabasamu, akaanza kumsogelea Daniel na kisha kumkumbatia. Hiyo ikaonekana kuwa faraja kwake, kumbatio ambalo alikuwa amelipata kutoka kwa Daniel likaonekana kumfariji na kumsahaulisha na Gibson kwa sekunde chache.
Baada ya hapo wakaanza kuongea mambo mengi ya nyuma ambayo yalikuwa yametokea katika maisha yao katika kipindi ambacho walikuwa wakiishi mitaani hata kabla ya Katie kujiingiza katika uchezaji wa filamu za ngono, hatua ambayo ilionekana kumuumiza sana Daniel ambaye alikuwa kwenye mapenzi mazito na Katie.
Daniel hakutaka kuwa nyuma, nae akaanza kumuelezea Katie kuhusu maisha yake toka siku ambayo walikuwa wametengana. Alimuelezea mambo mengi mpaka alivyokwenda nchini Uingereza na kutafuta fedha kwa nguvu mpaka kufikia hatua ya kuwa tajiri mkubwa. Historia zao zilionekana kufanana, walianzia maisha ya mitaani, maisha ambayo hayakuwa na ubora kabisa ila katika muda huo, wote walikuwa matajiri wakubwa.
Daniel hakutaka kukaa kimya, kwa wakati huo bado alikuwa akiona kwamba kulikuwa na uhitaji mkubwa wa kuzielezea hisia zake kwa msichana huyo, Katie na kwa jinsi moyo wake ulivyokuwa umeumia hasa mara baada ya kuona kwamba alikuwa ameolewa na mtu mwingine. Uso wa Daniel ulionyesha dhahiri kwamba alikuwa ameumizwa sana na tukio lile la ndoa na hivyo alikuwa akiomba Mungu kila siku kwamba awe tena na Katie kama ilivyokuwa zamani.
“Unafikiri Mungu amejibu maombi yako?” Katie aliuliza huku akimwangalia Daniel usoni.
“Yeah! Asilimia mia moja” Daniel alijibu huku akionekana kujiamini.
“Bado Daniel Itakubidi uombe sana. Unakumbuka kwamba nilikuacha ingawa ulikuwa kwenye mapenzi nami?” Katie alimuuliza Daniel.
“Ndio! Nakumbuka”
“Nilikuacha kwa sababu nilitaka kuwa huru zaidi ya jinsi nilivyokuwa. Sikuwa na fedha, nilikuwa nikishinda hata masaa kumi bila chakua. Nilitaka kuwa tajiri kama nilivyo kwa sasa. Nitazame sasa, ninaweza kula chochote ninachotaka, ninaweza kwenda popote ninapotaka kwenda. Nina kila kitu kwa sasa Daniel” Katie alimwambia Daniel.
“Ninafahamu. Lakini una maana gani kuniambia hayo yote?” Daniel aliuliza.
“macho yangu” Katie alimwambia Daniel.
“Ninakupenda Katie” Daniel alimwambia Katie.
“Macho yangu yanakwambia kila kitu” Katie alimwambia Daniel.
Daniel akasimama pale alipokuwa amekaa na kisha kuanza kumfuata Katie katika kochi alilokuwa amekaa na kisha kupiga magoti mbele yake. Tayari macho ya Daniel yalikuwa yamekwishabadilika, yakaanza kuwa mekundu kwa wakati huo.
Tayari macho ya Katie yalikuwa yamekwishamueleza kila kitu kwamba kwa wakati huo hakutaka kuwa nae. Kwa kiasi fulani Daniel akaonekana kuchanganyikiwa, alikuwa ametumia kiasi kikubwa cha fedha kwa kumtenganisha Katie na Gibson, sasa ingeleta maana gani kama nae pia asingekuwa na msichana huyo na wakati alikuwa ametoa zaidi ya dola milioni kumi.
Daniel aliona kwamba kulikuwa na kila sababu ya kulipigania penzi lake, aliona kwamba kulikuwa na kila sababu ya kumrudisha Katie katika mikono yake. Hakujali ni kiasi gani cha fedha ambacho angetumia kwa wakati huo, kitu ambacho alikuwa akikitaka ni kumuona Katie akirudi tena katika mikono yake kama ilivyokuwa zamani, nyakati zile walizokuwa wakiishi mitaani kama watoto wa mitaani.
Daniel akamshika Katie mkono huku akimwangalia usoni mwake. Macho ya Daniel yalikuwa yakionyesha kila dalili kwamba kwa wakati huo alikuwa akimhitaji sana Katie zaidi ya kitu chochote kile. Alipoona kwamba mguso wake mkono mwa Katie haukubalisha kitu chochote kile, akaupandisha na kuishika shingo ya Katie kwa mikono yake miwili.
“Ninakupenda”Daniel alimwambia Katie kwa mara nyingine tena.
Mawazo ya Katie yakaanza kurudi nyuma, tayari hali ya huruma ikaonekana kumuingia. Katika maisha yake, hakuwahi kumuona mwanaume akitoa machozi kwa ajili yake kama ilivyokuwa kwa Daniel katika kipindi hicho. Mawazo yake ya nyuma ndio ambayo yalikuwa yakiongeza chachu ya kuona kwamba kulikuwa na kila sababu ya kuwa na mwanaume huyo ambaye kwake alionekana kuwa mvumilivu kupita kawaida.
“Halikuwa chaguo langu sahihi” Katie alimwambia Daniel.
“Ninafahamu. Muache aende zake. Sahau kila kitu kuhusu yeye” Daniel alimwambia Katie.
“Vipi kuhusu kisasi?” Katie aliuliza huku akianza kulia.
“Hakuna uhitaji wa kufanya hivyo” Daniel alimwambia Katie.
Wote wakajikuta wakisimama na kisha kukumbatiana. Japokuwa kwa wakati huo lilikuwa jambo gumu sana kwa Katie kumsahau Gibson lakini akaona kulikuwa na kila sababu za kumsahau mwanaume huyo na kumuacha Daniel achukue nafasi ndani ya moyo wake. Mpaka kufikia hatua hiyo, tayari Daniel alikuwa akijiona kuwa mshindi, kiasi kikubwa cha fedha ambacho alikuwa amekitumia kilionekana kufanya kazi ile ambayo aliikusudia kufanyika.
Huo ndio ukawa mwanzo wa mahusiano yao ya kimapenzi kwa mara ya pili tena. Kila mmoja akaanza kumuahidi mwenzake kwamba angempenda mpaka pale ambapo kifo kingewatenganisha. Hakukuwa na mtu ambaye alikuwa akifikiria maisha ya baade yangekuwaje baada ya hapo, kitu walichokuwa wakikifikiria ni kufunga ndoa na kuishi pamoja hapo baadae.
****
“Unamaanisha mke wangu na mtoto wangu wamekufa” Gibson aliuliza huku akionekana kutokuamini.
Kila mmoja ndani ya ofisi ile akaonekana kumshangaa Gibson. Dokta hakuwa ameongea kitu chochote kuhusiana na mgonjwa wake lakini tayari Gibson akaonekana kufikiria jambo jingine zaidi. Hata kabla ya kuongea kitu chochote kile, dokta akaanza kuyafikiria maneno ya Gibson. Alijua na uhakika kwamba mgonjwa ambaye alikuwa ameletwa hospitalini pale ambaye alitekwa alikuwa mmoja, sasa huyo mtoto alitokea wapi?
Ingawa swali hilo lilianza kumtatiza kichwani mwake lakini dokta Mnyuzu hakutaka kuuliza kitu chochote kile zaidi ya kulifungua faili ambalo lilikuwa mezani mwake na kisha kuanza kuandika vitu fulani ambavyo hakukuwa na mtu yeyote ambaye alivifahamu.
“Mke wako ni mzima japokuwa hali yake ni mbaya sana” Dokta Myuzu alimwambia Gibson.
“Imekuwaje tena?”
“Hali inaonyesha kwamba alikuwa amekabwa kwa kipindi kirefu hali ambayo ilimfanya kutovuta pumzi kwa kiasi kikubwa, mbaya zaidi, kila alipokuwa akijaribu kuvuta pumzi, hiyo hivyo pumzi ndogo ambayo ilikuwa ikiingia, ilikuwa ikiingia na vumbi jingi” Dokta Mnyuzu alimwambia Gibson maneno ambayo yalionekana kumchanganya.
“Kwa hiyo hatopona?”
“Simaanishi hivyo. Kupona anaweza kupona japokuwa inaweza kuchukua muda mrefu kwani tumemuwekea mashine ya hewa ya oksijeni ili tuweze kuona maendeleo yake yatakuwaje?” Dokta Mnyuzu alimwambia Gibson.
“Nakuomba mponyeni mke wangu. Ninampenda sana, sitaki kumpoteza” Gibson alimwambia dokta Mnyuzu.
“Hata sisi hatutaki kumpoteza na ndio maana tunajitahidi kufanya kila tuwezacho kufanya kwa ajili ya kuirudisha afya yake kama ilivyokuwa kabla” Dokta Mnyuzu alimwambia Gibson.
“Na vipi kuhusu mtoto wangu?” Gibson aliuliza.
“Mtoto yupi?” Dokta Mnyuzu aliuliza huku akionekana kushangaa.
“Mtoto wangu, Genuine”
“Sijui kama kuna mtoto aliletwa hapa. Alikuwa na mkeo?”
“Ndio”
“Hapana. Mwanamke aliletwa peke yake” Dokta Mnyuzu alimwambia Gibson.
“Sasa mtoto wangu yupo wapi?” Gibson aliuliza.
“Mmmh! Sijui” Dokta alijibu.
“Kuna kitu nadhani kitakuwa kimeendelea. Maelezo yote juu ya mtoto tutayapata kutoka kwa wale watekaji” Manase aliwaambia.
Hawakutaka kuendelea kusubiri ndani ya ofisi ile, walichokifanya ni kuondoka na kuelekea katika chumba alicholazwa Prisca na kisha kumuangalia. Prisca alikuwa kimya kitandani, kwa kifupi alikuwa akionekana kama mtu ambaye tayari alikuwa amekwishakata roho. Gibson akasimama pembeni yake, tayari macho yake yalikuwa yamekwishaanza kutoa machozi, picha iliyoonekana kwa mkewe ikaonekana kumuumiza sana.
“Prisca mke wangu! Genuine yupo wapi?” Gibson alimuuliza Prisca huku machozi yakimtoka japokuwa alikuwa akifahamu kwamba Prisca asingeweza kujibu kitu chochote kile.
*****
Reuben, Filbert na Edward walikuwa chini ya ulinzi katika chumba kimoja kidogo huku tayari mawasiliano yakiwa yamekwishafanyika na makao makuu ya polisi ya jijini Dar es Salaam na hivyo watu hao walitakiwa kusafirshwa mpaka ndani ya jiji la Dar es Salaam.
Taratibu zote zilikuwa zimekamilika lakini mpaka muda huo ni kamanda Manase ndiye alikuwa akisubiriwa kutokana na kuwa na maswali machache na watu hao. Ilipofika saa kumi na mbili jioni, Manase akaingia katika kituo hicho na moja kwa moja kuelekea katika chumba kile na kuonana na watekaji wote watatu ambao walikuwa chini ya ulinzi wa polisi.
Kamanda Manase akaanza kuwaangalia kwa zamu, alipoona ameridhika, akakiweka chini kiti ambacho alikuwa ameingia nacho ndani ya chumba kile na kisha kutulia. Kwa wakati huo alikuwa akihitaji kufahamu kitu kimoja tu, sehemu alipokuwa mtoto Genuine ambaye hadi katika kipidi hicho hawakuwa wamemuona.
Reuben hakutaka kuficha, akaanza kuelezea kila kitu kilichokuwa kikihusiana na mtoto Genuine. Ilikuwa ni taarifa ambayo ilimhuzunisha sana Manase, hakujua namna ambavyo alitakiwa kuifikisha taarifa ile kwa Gibson ambaye alikuwa akitamani sana kusikia taarifa kuhusu mtoto wake wa pekee.
Manase hakutaka kukaa sana ndani ya chumba kile, alichokifanya ni kuanza kuelekea hospitalini ambako akamkuta Gibson akiwa ndani ya chumba kile huku akiendelea kuongea maneno mengi mbele ya uso wa mke wake japokuwa Prisca hakuwa amefumbua macho.
“Kuna taarifa nimepewa kuhusu mtoto wako” Manase alimwambia Gibson ambaye akamsogelea karibu huku akiwa na shauku ya kutaka kujua zaidi.
“Inasemaje?”
“Njoo nje kwanza” Manase alimwambia Gibson na kisha wote kuelekea nje.
Manase hakutaka kuficha kitu chochote kwa wakati huo, akamwambia Gibson kila kitu ambacho aliambiwa na Reuben ndani ya chumba kile. Gibson akauhisi mwili wake ukifa ganzi, akaanza kutetemeka huku hasira zikianza kumpanda.
“Unasemaje?”
“Hivyo ndivyo ilivyotokea. Kwa kweli imenihuzunisha sana. Huu ni unyama mkubwa sana kuwahi kutokea” Manase alimwambia Gibson.
Hiyo ilikuwa ni taarifa mbaya ambayo iliuumiza moyo wa Gibson kupita kawaida. Machozi yakaanza kutiririka mashavuni mwa Gibson, kile ambacho alikuwa amekisikia kiliuchoma sana moyo wake. Akalifuata benchi na kisha kulikalia huku akikiinamisha kichwa chake chini.
Taswira ya mtoto wake ikaanza kumjia kichwani, alikumbuka mambo mengi kuhusiana na mtoto wake, akalikumbuka tabasamu lake, akaanza kukikumbuka kicheko chake hasa pale ambapo alikuwa akimfanyia vitu ambavyo vilikuwa vikimfanya kucheka.
Katika kila kitu ambacho alikuwa akikifikiria kwa wakati huo kilikuwa kikizidi kumuumiza moyo wake kupita kawaida. Mtoto wake ambaye alikuwa akimpenda sana, kwa wakati huo hakuwa pamoja nae tena, alikuwa ameuawa katika kifo kibaya ambacho kila mtu ambaye angesikia, angeumia moyoni.
Wakati mwingine, alihisi kuisikia sauti moyoni mwake, sauti ambayo ilikuwa ikisisitiza kwamba kila kitu ambacho kilikuwa kimetokea yalikuwa ni matunda ya vitu ambavyo alikuwa amevipanda kabla. Kwa wakati huo ulikuwa muda wa mavuno wa yale ambayo alikuwa amepanda siku za nyuma.
Usaliti ambao alikuwa ameufanya kwa mke wake, Prisca ndio ambao ulikuwa umeleta matatizo yale yote. Alijua fika kwamba kama asingekuwa amemsaliti mke wake, Prisca basi kwa wakati huo asingekuwa katika wakati mgumu kama ambavyo alivyokuwa kwa wakati huo.
“Ila mimi ndiye niliyesababisha haya yote” Gibson alimwambia Manase.
“Najua. Ila kwa sasa hautakiwi kujilaumu. Kila kilichotokea, kimetokea” Manase alimwambia Gibson.
“Nafahamu. Ila naamini kama nisingekuwa nimemsaliti Prisca kipindi cha nyuma, nina uhakika hata jambo hili lisingetokea kwa sasa. Usaliti wangu umenigharimu sana katika maisha yangu. Usaliti ambao niliufanya kipindi kile, hizi ndizo athari zake. Ninajuta kumsaliti mke wangu” Gibson alimwambia Manase ambaye alikuwa kimya kumsikiliza.
“Fedha zilinifanya nimsaliti mke wangu. Hizi hizi fedha haziwezi kunirudishia mtoto wangu. Huu umekuwa ni kama msumali wa moto ndani ya moyo wangu, tukio hili limeniachia kidonda kikubwa moyoni, kidonda ambacho sidhani kama kuna siku kitakuja kupona” Gibson alimwambia Manase.
“Usijali Gibson. Kila kitu ni mipango ya Mungu”
“Hapana. Vitu vingine si mipango ya Mungu. Mungu hakupanga nimsaliti mke wangu, Mungu hakupanga nisafiri kwenda nchini Marekani na kufunga ndoa na msichana Katie. Hii ilikuwa mipango yangu, tamaa zangu za kutaka fedha ndizo ambazo zimenifanya niwe katika hali hii kwa sasa” Gibson alimwambia Manase huku akitokwa na machozi.
“Usilie Gibson. Jikaze. Wewe ni mwanaume” Manase aliendelea kumbembeleza Gibson.
“Kujikaza ni vigumu sana. Inaniuma sana kumpoteza mtoto wangu ambaye nilikuwa nikifanya mambo mengi kwa ajili yake. Inawezekana mtoto wangu angekuwa rais, inawezekana mtoto wangu angekuwa waziri mkuu. Ndoto zake za kufikia mafanikio zimefutika kwa sababu ya tamaa zangu za kutamani sana fedha. Nilichokuwa nikikifikiria ni fedha tu, sikutaka kufikiria ni kitu gani kingetokea baada ya hapo. Moyo wangu unajuta, sijui ni kwa namna gani nitakuwa nikiishi na mke wangu bila ya kuwa na mtoto wetu. Nadhani yatakuwa maisha yatakayoniumiza sana, nadhani yatakuwa ni aina ya maisha ambayo yatanifanya kukosa amani na furaha ndani ya moyo wangu” Gibson alimwambia Manase ambaye alibaki kimya huku nae akianza kuyafikiria maneno ya Gibson.
Gibson aliongea maneno mengi tena kwa sauti ya unyonge. Ingawa maneno yalikuwa mengi lakini hayakuweza kubadilisha kitu chochote kile, ukweli ulibaki vile vile kwamba Genuine alikuwa ameuawa kinyama.
Kila kitu kikapangwa na kisha baada ya siku moja safari ya kurudi jijini Dar es Salaam kuanza. Gibson hakutaka kumuacha mke wake ahudumiwe mkoani Tanga jambo lililompelekea kumsafirisha kuelekea jijini Dar es Salaam kwa kutumia usafiri wa ndege. 


Je nini kitaendelea Fuatilia sehemu ya mwisho kesho saa MOJA  USIKU.
Imedhaminiwa na  dick sound,masa celagem.,husein pamba kali,facebook take away,1 ted na zanel bongo ladies wear.

IGIZO JIPYA LINAFATA LA KAHABA TOKA CHINA.

No comments:

Post a Comment